ATHARI ZA UHARIBIFU WA MISITU AMBAZO HAZIKO WAZI SANA
Misitu ni uhai kama inavojulikana na watu kwa asilimia kubwa
na pia ikiwa ndio kauli mbiu ya wakala wa huduma za misitu Tanzania TFS. Zamani uhitaji wa kupanda miti haukuwepo
kutokana na kuwa misitu ilikuwa mingi na matumizi yalikuwa yako chini kutokana
na idadi ya watu lakini pia maendeleo yanayohitaji bidhaa hizi za misitu kama
malighafi za kuzalishia bidhaa hizo. Kwa kipindi tulichopo sasa kutokana na
hali halisi kubalika tumeingia katika janga la kupoteza misitu kwa asilimia
kubwa sana na hali hiyo kupelekea kuwa na mabadiliko ya tabia nchi hivyo
kupelekea kuwa na mikakati ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi
ikiwa ni pamoja na upandaji wa miti kwa kiasi kikubwa na kulida misitu ile
ambayo bado imesalia kusudi isiweze kuvamiwa tena. Na ahgenda hii imekuwa ya
kimataifa kwani na Afrika kuwa mhanga mkubwa wa mabadiliko ya tabia nchi lakini
nchi nyingine zote duniani nazo zanpatwa na madhara hayo kwa namna moja au
nyingine.
Athari za mabadiliko ya tabia nchi ambayo husababishwa na
uharibifu wa mazingira hasa uharibifu wa misitu ambazo wengi tunazifahamu ikiwa
ni pamoja na kukosekana kwa mvua ambayo husababisha ukame mkubwa na kukausha mimea
lakini pia kuharibu makazi ya viumbe hai kama ndege na vinginevyo. Joto
kuongezeka na kusababisha mgonjwa ya Ngozi na madhara mengine ambayo hayakuwepo
kabla, ongezeko la wadudu katika kilimo inayopelekea wakulima wa hali ya chini
licha ya kuathiriwa na ukame ila hata kule kidogo ambacho wanakipata huharibiwa
na wadudu na kufanya kuwa na uhitaji wa chakula kwa kiasi kikubwa.
Pamoja na athari zote hizo ila kumekuwa na athari moja
ambayo ni kubwa ila watu wanashindwa kuitambua kwa urahisi kuwa nayo pia ni
kutokana na uharibifu wa mazingira hasa katika eneo la uoto wa asili
“Biodiversity” hili ni eneo muhimu sana katika kukamilisha kitu tunachoita
msitu. Labda tukumbushane tofauti ya hizi aina mbili za misitu na kwann
zikatengwa kuwa ni vitu viwili tofauti. Misitu ya asili na misitu ya kupandwa,
misitu ya asili maana yake ni miti iliyofungana lakini pia chini kuna uoto
unaofunika ardhi “trees with vegetation cover” na msitu wa kupandwa ni miti
iliyopandwa kwa nafasi na kupaliliwa na hivyo kukosekana ule uoto unaofunika
ardhi.
Aina zote mbili za misitu zinafaida ya kuleta mvua,
kukabiliana na tatizo la ongezeko la joto, kunyonya hewa chafu inayotoka
viwandani na kupendezesha mazingira yetu. Faida ambayo misitu ya asili inaizidi
misitu ya kupandwa ni ile ya uwepo wa uoto wa asili unaofunika ardhi. Hii faida
yake huonekana pale mvua inaponyesha utaona katika msitu wa kupandwa maji
yanayotiririka ni mengi kuliko maji yanayotiririka katika msitu wa asili.
Tofauti hii husababishwa na katika msitu wa asili tone linapodondoka
linalazimishwa kuzama chini kwani halipati nafasi ya kuungana na matone mengine
kutengeneza maji mengi na kuanza kutembea ila katika misitu ya kupandwa tone
linapodondoka linaruka na kupata nafasi ya kukutana na tone jingine na hivyo
kutengeneza maji na kuanza kutembembea kuelekea mteremko ulipo na mwisho wa
siku hutengeneza mfereji na mwisho korongo na kuleta mafuriko huko mabondeni.
Hata hivyo kinachosikitisha sana kwa sasa hata hii misitu ya
asili asilimia kubwa imekuwa kama misitu ya kupandwa na kuwa na tabia za misitu
ya kupandwa japo inaundwa na misitu ya asili. Hii yote imetokana na shughuli za
kibinadamu zinazofanyka katika misitu hiyo ikiwa kubwa Zaidi ni ufugaji na
uchungaji wa mifugo unaoharibu kwa kiasi kikubwa uoto huo wa asili unaofunika
ardhi. Hivyo unaweza pita kwa mbali ukaona miti imefunga vizuri ukajua hapo
kuna msitu mzuri wa asili lakini ukisogea karibu unakutana na ardhi ikiwa uchi
na kuondoa maana yote ya msitu wa asili na kuwa kama msitu wa kapandwa tu.
Kwa mujibu wa wazee wa zamani ambao bado wapo wanasema kuwa
hawajashtushwa na mvua hizi kubwa zinazoendelea kunyesha kwa sasa ila
kinachowashangaza ni mafuliko yanayotokea kwani hawajawahi kuyashuhudia kabla
maana mashamba yanajaa maji n ahata kilimo kimekuwa changamoto kubwa kwao.
Wanasema hata mwaka 1998 iliponyesha mvua kubwa ya elninyo maji hayakuwa mengi
kiasi hiki ila kwa hii ya mwaka huu imekuwa ya kushangaza kidogo kwao. Hapa ndo
unagundua sasa kuwa uharibifu wa uoto wa asili umechangia kiasi kikubwa katika
kusababisha maji kutiririka kwa kasi kutoka milimani na kusambabisha mafuriko,
uharibifu wa miundo mbinu na majanga mengine mengi.
Ufugaji ni mzuri na una tija kwa wananchi wenyewe na pia kwa
taifa kwa ujumla kama ukifanywa kwa kuzingatia usalama wa mazingira yetu
hususani katika misitu yetu ya asili. Lakini kama tusipolifanyia kazi hili
mapema tutegemee kila mvua zitakapokuwa zinanyesha basi kutakuwa na madhara
kadha wa kadha kwa wananchi na hata kwa serikali kwa ajili ya kutengeneza
miundo mbinu inayoharibiwa na mvua kila wakati.
Rai yangu kwa mamlaka zinazohusika tunajitahidi kuhamasisha
watu kupanda miti ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi tusisahau
kuilinda misitu ya asili na uoto wake kwa vyote vina umuhimu mkubwa sana kwa
maendeleo ya taifa na wananchi wake kwa ujumla. Hivyo kila mtu apande miti mingi
kadri anavoweza lakini pia tuwajibike wote katika kuitunza misitu ya asili
iliyopo kusudi kuepukana na haya yote yanayotokea sasa hivi.
Mungu ibariki
Tanzania,
Mungu ibariki Afrika.
Imeandika na Martin
Njau,
0717599375/0753989840 njaumartin48@gmail.com
Mwanaharakati wa
mazingira na bwana Misitu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni