Jumapili, 10 Septemba 2017

BORA MOJA YENYE FAIDA KULIKO KUMI INAYOUMIZA.





“MDA  MWINGINE NI BORA KUOKOTA NA KUBEBA MOJA YENYE FAIDA NA MANUFAA KWAKO KULIKO KUKUMBATIA KUMI INAYOKUUMIZA NA KUKURUDISHA NYUMA”

Kama ilivyo ada ya safu yetu ya kujuzana moja na mbili ili hali ni katika kubadilishana mawazo na kuongezeana uelewa katika baadhi ya mambo ya kimaisha. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kutujalia afya mjema na nguvu nyingi kwa ajili ya utukufu wake. Lakini pia kwa ajili ya kutufanya tuendelee kutimiza wajibu wetu kama wanadamu. Ni matumaini yangu kuwa u mzima wa afya na unaendelea vizuri na majukumu yako, kama huko poa basi Mungu akujalie upate nafuu mapema. Karibu tena katika safu yetu ya kujuzana. 

Mada ya leo inahusu kuachia vitu ambavyo kwa wakati mwingine huwa havina faida kwetu. Mada inasomeka hivi “mda mwingine ni bora kuokota na kubeba moja yenye manufaa na faida kwako kuliko kukumbatia kumi inayokuumiza na kukurudisha nyuma”. Mara nyingi tumekuwa tukishikilia vitu ambavyo huwa havina manufaa kwetu ila kutokana na kuwa na matumaini potofu au matumaini yaliyokufa ambayo hayana macho tunajikuta tukiendelea kuyakumbatia tena kwa mikono miwili. Hii ni kawaida kwa kila mtu na hutokana na labda mtu huyo alikuwa na matarajio flani juu ya kitu hicho lakini kiukweli ni kwamba uwezekano wa kupata au kufanikiwa kufikia matarajio yake ni hafifu sana. Lakini kutokana na woga wa kwamba inawezekana ni nyundo ya mwisho jiwe litapasuka lakini unajikuta bado sana na kuzidi kupoteza muda juu ya hilo.
Kiukweli watu wengi wanakuwa na maumivu hasa ya ndani kwa ajili ya hilo kwani watu wanahifadhi vitu ambavyo kiukweli havina faida yoyote na kuna uwezekano wa kwamba vitu hivyo vinaendelea kumuumiza mtu na anashindwa kuviacha kutokana na kile kinachozaniwa kuwa labda mafanikio yapo karibu na unajipa moyo wa kuendelea kusubiri tena. Sisemi kuwa ni kosa kufanya hivyo ila kuna kila sababu ya kubadilika na kuanza upya kwani kufanya hivyo ni sawa na kusubiria mbegu iliyooza iweze kuota kitu ambacho ni upotezaji wa mda. Kinachotakiwa ni kuifukua na kupanda nyingine kana kwamba hiyo haitoshi basi pia ni lazima uangalie ni kitu gani ambacho kimesababisha kuweza kuoza kwa mbegu hiyo. 

Ukimuuliza mtoto kati ya moja na kumi kubwa ni ipi lazima atakujibu kuwa ni kumi ndo kubwa. Lakini unapomuuliza mtu mzima kati ya moja na kumi ipi kubwa kama anafikiria vizuri basi atakuuliza katika upande gani? Maana kuna wakati kumi inakuwa kubwa na wakati mwingine moja inakuwa kubwa zaidi ya kumi kutokana na eneo ambalo imetumika. Hii ina maana kuwa kuna wakati inabidi kuachia kumi ambayo inakuwa haina faida kwa wakati huo na kuokota moja ambayo ina faida na maendeleo bora kwako.

Marafiki ni vizuri kuwa nao ila unapoona kuwa upo na marafiki ambao sio sahihi ni bora kuwaachia na kutengeneza nafasi kwa ajili ya marafiki ambao wanafaida kwako na wanakusaidia kufikia malengo yako na kukushauri pale unapokosea. Pia kama rafiki lazima awe anajali na kuona ya kuwa ana kila sababu ya kukufanya ujisikie kuwa rafiki yake kwani unaweza kuwa na rafiki lakini usiweze kuhisi uwepo wa huyo rafiki yako kwani mchango wake unakuwa mdogo sana kwako.kuwa rafiki sio jina tu kuwa flani ni rafiki yangu ila je kuna vitu vyovyote ambavyo vinaonesha uhalisia wa urafiki wenu? Urafiki ni zaidi ya jina. Kubeba watu ambao hawana faida maishani mwako ni uzembe na uvivu wa kutafuta marafiki wenye tija katika maisha yako. Ni sawa na kuogopa kwenda shamba eti kisa mvua inanyesha. 

Tengeneza nafasi kwa ajili ya marafiki walio na tija katika maisha yako achana na kukumbatia marafiki ambao hawana maana katika maisha yako kwani wanaweza kuwa wanakuchelewesha kule unakoenda na mwisho wa siku kumbe hawaendi huko. Na baada ya hapo ni kukucheka kuwa muone alivyoaibika alikuwa anajifanya anaweza sana kumbe hamna kitu. Kaa mbali nao sana kwani sio watu wazuri hata kidogo kwa maendeleo ya afya yako ya kimaendeleo. Fanya mabadiliko sasa ya kuacha kukumbatia vitu ambavyo havina  faida kwetu na vinatupotezea muda. Sasa ni muda sahihi wa kukaribisha vitu ambavyo vina faida kwetu hata kama vinaonekana kuwa vidogo ila vina faida kuliko kukumbatia hivyo vikubwa lakini havina faida.
Njau M
0717599375

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni